Taarifa kwa Vyombo vya Habari

Mpango wa Miaka 10 mfumo wa uchumi wa Kidijiti (DEF) wakamilika

Mpango wa miaka 10 mfumo wa uchumi kidijiti (DEF) wakamilika

Baraza la Taifa la Biashara (TNBC), kupitia Kikundi Kazi chake cha Kidijiti chini ya Mwenyekiti wake ambaye ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Mohamed Abdulla imepitisha mpango wa miaka 10 wa mfumo wa uchumi wa Kidigiti wa  Kitaifa (DEF)

Akizungumza mara baada ya kikao cha Kikundi cha Kidijiti jijini Dar es salaam, Dkt. Abdulla amesema baada ya kupitisha kazi iliyopo mbele yao ni kuandaa andiko litakalo zinduliwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Mwenyekiti wa TNBC.

“  Mpango huu utatoa taswira kwa uongozi kuwa nini kifanyike ili kuweza kuhakikisha uchumi wa Kidijiti unakuwa na manufaa kwa Taifa kwani kuna mambo mengi tuliyo yaangazia na kuyaboresha katika mpango huu hivo utekelezaji wake utakapo anza utakuja na mafanikio kwani Watalaamu wamechambua na kutoa maoni yenye tija kwa Taifa’’ alisema Dkt. Abdulla

Pia Dkt. Abdulla amesema kuwa mpango kazi uliopitishwa na Wajumbe wa jopo hilo utapelekwa mbele ya Mwenyekiti wa Balaza hilo ambaye ni  ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ili uweze kuzinduliwa rasmi mwezi wa kwanza.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara, Dkt. Godwill Wanga   alisema kuwa uchumi wa kidijiti utasaidia kupunguza gharama za ufanyaji Biashara na hivyo kukuza pato la Mtanzania na Taifa kiujumla.

‘’Kupitia mpango huu kuna mambo mengi ambayo tumeyajadiri na Wajumbe ikiwa ni pamoja na mahitaji ya rasilimali watu yatakayo hitajika kukuza uchumi wa Kidijiti , sambamba na  kuangazia Taasisi  muhimu zitakazo jengewa uwezo ili zikatoe mchango stahiki katika kufikia malengo ya Taifa katika uchumi wa kidijiti’’ alisema Dkt. Wanga

Aidha aliongeza kuwa miongoni mwa maazimio yaliyopitishwa na Wajumbe ni pamoja na matumizi ya teknolojia mbalimbali pamoja na miundombinu itakavyowezesha  kukuza uchumi wa Kidijiti hapa nchini.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Azam Media, Bw. Tido Mhando  alisema Kikundi Kazi hicho kwa kushirikiana na vyombo vya habari watahakikisha wanatoa mchango stahiki ikiwa ni pamoja na   utoaji wa  elimu kwa Wananchi kuhusu matumizi ya TEHAMA  ili kutimiza azma ya Serikali ya kuchochea  ukuaji wa uchumi  wa Kidijiti kwa maendeleo ya kijamii.

“ Mikakati ya Serikali ya kuimarisha sekta ya TEHAMA na mawasiliano hapa nchini inaonekana kwa vitendo  kwani  imekuwa ikishirikisha Sekta Binafsi kikamilifu hivyo  kupitia ushirikiano huu hakika tunaenda kuleta mapinduzi  katika kukuza maendeleo ya uchumi wa kidigiti hapa nchini , alisema Bw. Mhando.

Afisa Mtendaji mkuu wa Multi Choice Tanzania, Bi. Jacqline Woiso alisema watashirikiana kwa karibu na wadau wa elimu katika kuhakikisha Vijana wanashiriki kikamilifu katika kuchochea ukuaji wa maendeleo ya Kidigitali nchini.

 “Kupitia mpango huu tutaenda kujenga sambamba na kukuza vipaji vya Vijana wetu  kwa kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Elimu pamoja na Wadau wa Elimu katika kuhakikisha vijana wanajengewa uwezo utakaosaidia kukuza maendeleo ya Kidigitali na kuleta tija kwa Taifa , alisema Bi. Woiso